1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaAsia

UN yastushwa na sheria ya maadili ya Afghanistan

Hawa Bihoga
25 Agosti 2024

Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Afghanistan umesema leo kuwa una wasiwasi kuhusu sheria ya maadili iliyoidhinishwa hivi karibuni na serikali ya Taliban, ukikosoa hasa vipengee vinavyowadhibiti wanawake.

https://p.dw.com/p/4jtol
Kabul, Afghanistan | Wanawake wakiandamana
Wanawake wa Afganistan wakiandamana mjini Kabul AfganistanPicha: Bilal Guler/AA/picture alliance

Mnamo Jumatano, serikali  ya Afghanistan ilitangaza uanzishaji wa sheria yenye vifungu 35 inayoelezea kwa kina miongozo ya tabia na mtindo wa maisha vinavyozingatia tafsiri yake ya Sheria ya Kiislamu. 

Sheria hiyo inaweka adhabu za hatua kwa hatua za ukiukaji, kuanzia maonyo ya madomo hadi vitisho, faini na vifungo vya urefu tofauti, zinazotekelezwa na polisi wa maadili waliyoko chini ya Wizara ya Uenezaji wa Maadili na Kuzuwia Maovu. 

Soma pia:Taliban yamzuia mtaalamu wa UN kuingia Afghanistan

Mkuu wa Ujumbe wa Msaada wa Umoja wa Mataifa nchini Afghanistan, UNAMA, Roza Otunayeva, amesema ni maono yanayotatiza kwa Afghanistan, ambapo wakaguzi wa maadili wana mamlaka ya hiari kutisha, na kumuweka kizuwizini mtu yeyote kwa msingi wa orodha ndefu ya ukiukaji, ambayo wakati mwingine haiko wazi.