1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mahakama ya Haki Afrika mashariki yapata jaji mpya

5 Septemba 2024

Mahakama ya Afrika ya Haki za binadamu yenye makao yake makuu mjini Arusha, Tanzania, imemuapisha jaji mpya.

https://p.dw.com/p/4kK6y
Mahakama ya haki za binadamu ya Afrika Mashariki iliyoko Arusha  Tanzania
Mahakama ya haki za binadamu ya Afrika Mashariki iliyoko Arusha TanzaniaPicha: Veronica Natalis/DW

Jaji huyo mpya raia wa Jamhuri ya Uganda Duncan Gaswaga, amechukua nafasi ya jaji Ben Kioko kutoka nchini Kenya aliyemaliza muda wake wa kisheria baada ya kuitumikia Mahakama hiyo kwa kipindi cha miaka 12.

Jaji Duncan ambaye amebobea katika sheria ya kimataifa ya makosa ya jinai na haki za binadamu anakuwa jaji wa sita ambaye anazungumza lugha ya kingereza katika mahakama hiyo ya Afrika, inayotumia lugha nne mpaka sasa ambazo ni Kingereza, Kifaransa, Kiarabu na Kireno.

Rais wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu Jaji Amani Aboud, amewaambia waandishi wa habari kwamba kuapishwa kwa jaji Duncan kutaleta uzoefu mpya wa kuzitafsiri sheria na kutoa maamuzi mbali mbali yanayohusu haki za binadamu barani Afrika.

Japo Mahakama hiyo yenye majaji 11, inakabiliwa na changamoto ya kutotekelezwa kwa maamuzi yake, imessitiza itaendelea kujizatiti kuhakikisha nchi wanachama zinaheshimu haki za binadamu.